Siku ya Wanawake wa Vijijini ilianzishwa mwaka 2008 kwa lengo maalum la kutambua mchango wa wanawake wa vijijini katika maendeleo ya kilimo, maendeleo ya vijijini, na kuondoa umasikini katika jamii zetu sambamba na kukabiliana na changamoto wanazopitia.
Watu wa vijijini hasa wanawake ni muhimu sana katika kuleta maendeleo na kuondoa umasikini lakini ndio kundi ambalo limekuwa likikosa kipaumbele. Ukosefu wa huduma mbalimbali vijijini ikiwemo ajira, huduma bora za afya, elimu, umeme, maji na uhafifu wa miundombinu hufanya watu wengi kuhamia au kutamani kuhamia mijini. Kutokana na mabadiliko mbalimbali ya kijamii kisiasa na kiuchumi kuna haja kubwa ya kuangalia mahitaji na umuhimu wa kulinda wanawake na wasichana wa vijijini lakini zaidi kutambua mchango wao mkubwa na kuweka mazingira wezeshi ya kuwawezesha kusonga mbele.
Wanawake wa vijijini ni zaidi ya robo ya watu wote duniani ambapo asilimia 43% hujishughulisha zaidi na kilimo hasa katika nchi zinazoendelea. Katika idadi ya wanawake nchini Tanzania asilimia 77.9% ni wanawake wa vijijini na 22.1 ni wanawake wa mijini. Wanawake na wasichana wengi wa vijijini hawana elimu na hawawezi kuingia katika ushindani wa ajira na pia wamekuwa wakiathiriwa zaidi na mila na desturi na kutokuwa na usawa wa kijinsia vitu vinavyoongeza vikwazo katika kufikia haki pale wanapofanyiwa vitendo vya kikatili.
Muundo wa kisheria
Hakuna sheria maalumu nchini Tanzania ya kulinda wanawake wa vijijini lakini Tanzania imetia saini mikataba ya kimataifa ikiwemo Mkataba wa Kupinga Aina Yoyote ya Ubaguzi Dhidi ya Wanawake (CEDAW) pamoja na Mkataba wa Nyongeza wa Haki za Wanawake wa Afrika (Maputo protocol) ambayo yote imetoa vifungu maalum vya kutetea haki za wanawake wa vijijini.
Ibara ya 14 ya Mkataba wa Kimataifa wa Kupinga Aina Yoyote ya Ubaguzi Dhidi ya Wanawake inataka nchi wanachama kuangalia kwa kina matatizo wanayokutana nayo wanawake wa vijijini na mchango wao katika jamii na kuhakikisha haki zao zinalindwa. Mkataba huo umeenda mbele zaidi na kusema kuwa nchi wanachama zihakikishe kuwa wanaondoa aina zozote za ubaguzi dhidi ya wanawake wa vijijini ili kuhakikisha kuna usawa kati ya wanawake na wanaume na kuwa wanawake wa vijijini wanashirikishwa ipasavyo na wananufaika katika maendeleo ya nchi yao. Kwa kufanya hivyo nchi wanachama watahakikisha kuwa wanawake wa vijijini wanashirikishwa na wanaeleweshwa kuhusu mipango ya maendeleo, wanapata huduma ya afya ipasavyo, wananufaika kutokana na huduma mbalimbali za kijamii, wanapata elimu na mafunzo mbalimbali kuhusu maisha na maendeleo yao, wanaanzisha vikundi mbalimbali vya maendeleo ili kupata nafasi sawa katika ajira na biashara, wanashiriki na kushirikishwa katika shughuli za jamii, wanapata nafasi kupata mikopo na masoko kuhusu bidhaa zao za kilimo, wanafurahia maisha bora katika viwango vinavyofaa.
Mwaka 2016 kamati ya CEDAW ilitoa mapendekezo ya jumla namba 34 ambayo yaliomba nchi wanachama kuhakikisha haki za wanawake na wasichana wa vijijini kuhusu ardhi, usawa wa kijinsia na usalama wao vinapewa kipaumbele.
Japo Tanzania imechukua juhudi za makusudi kuhakikisha tunafikia usawa wa kijinsia, bado wanawake wa vijijini wamekuwa wakipitia changamoto nyingi ambazo zinahitaji juhudi zaidi kuweza kusaidia. Changamoto hizo ni pamoja na sheria kandamizi hasa katika masuala ya mirathi na ndoa, kutokuwa na usawa katika upatikanaji wa masoko na umiliki ardhi vijijini, mila na desturi zilizopitwa na wakati ikiwemo ukeketaji ambao kwa vijijini ni asilimia 13.1 ukilinganisha na mijini ambapo ni aslimia 5.5.
Changamoto nyingine ni pamoja na mfumo dume ambao umeshamiri sana vijijini, ukosekanaji wa huduma bora za afya , ukosekanaji wa elimu bora na mwamko wa elimu hiyo, kukosekana kwa wanawake wengi kutoka vijini katika ngazi za maamuzi na uongozi, ajira kwa watoto hasa wa kike, ukosefu wa ajira na changamoto nyingine nyingi ikiwemo zaidi ukatili wa kijinsia ambao umeshamiri sana kila mahali na zaidi vijijini, ukosekanaji wa haki kutokana na kutokuwa na elimu kuhusu haki zao.
Mapendekezo kwa lengo la maboresho
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu tunaamini kwamba usawa wa kijinsia utaharakisha maendeleo hasa vijijini ambapo kuna idadi kubwa ya wanawake. Jamii inapaswa kuamini katika usawa ili kuwapa wanawake fursa sawa na kutambua mchango wao.
#AminiaUsawa
Imetolewa na; Kituo cha Sheria na haki za Binadamu pamoja na Mtandao wa kupinga Ukeketaji Tanzania.
Unleash your inner purpose to help the helpless, marginalized and oppressed. Your contribution will help our course in provision of legal aid and promotion of human rights.
Help us curb human rights violations such as the murderous attack against people with albinism and elders.
Your donation will help us empower the general public with civic education on cross cutting issues counting gender issues and democracy to realize the changes we aspire.
Help us safeguard human rights all together.
Huenda huna muda wa kutosha wala kipato cha kutosha kulinda utu na haki za wengine, ingawa unawiwa kufanya hivyo.
Ni jukumu letu sote kujitoa kwa kidogo tulichojaaliwa ili kupaka rangi ya furaha katika nyuso za wengine, wewe, yule na sisi tukikusanya nguvu tunaweza kutetea na kulinda haki za wanaoonewa kwa kushindwa kuzifikia huduma za haki.
Jitolee sasa kidogo ulichonacho kusaidia ulinzi na utetezi wa haki na utu wa binadamu.
LEAVE A REPLY
Your email address will not be published.